BODI YA MIKOPO YAWAPA AHUENI YA MUDA WADAIWA WAKE KUREJESHA MADENI YAO
Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu imeongeza muda kwa wadaiwa sugu kulipa madeni yao hadi Desemba 30, 2016.
Hatua ya Bodi inafuatia mwitikio chanya kutoka kwa wadaiwa ndani ya siku 30 za awali ambazo zinakamilika leo Desemba 14, 2016.
Akitoa taarifa ya kuongezwa kwa muda; Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi,
Abdul_Razaq Badru amesema kuwa wadau wameomba kuongezewa muda kutokana
na baadhi yao kukabiliana na changamoto za majukumu ya kazi na hivyo
kushindwa kujitokeza ndani ya siku 30 zilizokuwa zimetangazwa awali.
Katika hatua nyingine, Bw. Badru amesema kuwa ndani ya siku za nyongeza
Ofisi za Bodi ya Mikopo zilizopo Mwenge, jijini Dar es Salaam
zitaendelea kuwa wazi kwa siku za Jumamosi, Disemba 17, 2016 na
Jumapili, Disemba 18, 2016 kuanzia saa 3:00 asubuhi hadi saa 9:00
alasiri ili kutoa fursa muhimu kwa wadaiwa wote wa mikopo ya elimu ya
juu ambao hawajaanza kurejesha mikopo yao kupata taarifa kuhusu madeni
yao na kulipa.
Ili kuharakisha utoaji wa muhtasari wa deni la mdaiwa; mhusika aje na
Majina yake kamili, Chuo alichosoma, Mwaka wa kuanza na wa kuhitimu,
anuani yake ya barua pepe (email), nambari ya simu ya kiganjani, mwajiri
wake na Check Number yake iwapo ameajiriwa serikalini.
‘Kuwa Mzalendo, Rejesha Mkopo wa Elimu ya Juu’
Kwa mawasiliano zaidi piga 0763 459165 au 0767 513208
Imetolewa na:
MKURUGENZI MTENDAJI
BODI YA MIKOPO YA WANAFUNZI WA ELIMU YA JUU
14/12/2016
Leave a Comment