OBAMA AMUONYA TRUMP KUWA HATOKAA KIMYA ENDAPO ATAVUNJA MISINGI YA URAIS
Rais mteule Donald Trump akiwa na Rais anayemalizia madaraka Barrack Obama
Rais wa Marekani anayeondoka Barack
Obama amesema huenda akazungumza, kinyume na utamaduni wa siasa
Marekani, iwapo mrithi wake Donald Trump atatishia "maadili muhimu" ya
Marekani.
Huwa desturi kwamba marais wa zamani wa Marekani huwa
hawajiingizi sana katika siasa baada ya kuondoka madarakani na huwa
hawazungumzi kuhusu warithi wao.
Akiongea katika kikao na
wanahabari wakati wa mkutano wa nchi za Asia na Pasifiki (Apec) mjini
Lima, Peru, Bw Obama amesema anakusudia kumsaidia Bw Trump na kumpa muda
wa kueleza maono yake.
Lakini amesema kwamba, kama raia, huenda akalazimika kuzungumza kuhusu baadhi ya mambo.
"Ninataka kuiheshimu ofisi na kumpa rais mteule fursa ya kueleza
msimamo wake na mipango yake bila mtu kujitokeza kumkosoa," Bw Obama
alisema.
Lakini akaongeza, kwamba iwapo suala "litagusa maadili
muhimu ya Marekani na imani yetu, na nafikiri kwamba inahitajika au
itafaa kwangu kutetea maadili hayo, bado nitalitathmini wakati huo".
Kisha, amejieleza kama "raia wa Marekani anayejali sana taifa"
Bw Obama amekihutubia katika kikao na wanahabari mkutano wa Apec mjini Lima, Peru



Leave a Comment